JINSI YA KUEPUKA KUFIKILIA NGONO MUDA WOTE SOMA HAPA,,,,,,,,,,
”
Je, wewe hutumia saa nyingi
ukiwaza juu ya watu wa jinsia tofauti, kama anavyofanya Michael? Ikiwa
ndivyo, huenda ukahisi kana kwamba unapigana vita na akili yako. Fikira
za ngono huingia akilini mwako kama jeshi la adui. “Fikira hizo zinaweza
kukutawala,” asema Michael. “Zinaweza kukufanya uzunguke njia ndefu ili
tu umtupie jicho msichana fulani mrembo, au kutembea-tembea dukani
wakati ambapo hukusudii kununua chochote ili tu umtazame mtu fulani kwa
ukaribu.”
Hata hivyo, kumbuka kwamba kuwa
na hisia za ngono si dhambi. Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke
wakiwa na uvutano wenye nguvu kati yao, na hakuna ubaya wa kutosheleza
tamaa za ngono katika mpango wa ndoa. Kabla ya kufunga ndoa, huenda
ukawa na tamaa kali za ngono. Hilo likitokea, usidhani kwamba wewe ni
mtu mwovu au kwamba huwezi kuishi maisha safi. Unaweza kudumisha usafi wa kiadili ukiamua kufanya hivyo! Lakini ili ufanikiwe, utahitaji kudhibiti mawazo yako kuhusu watu wa jinsi tofauti. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani?
Angalia watu unaoshirikiana nao.
Wanafunzi wenzako wakianza kuzungumzia mambo ya ngono, huenda ukataka
kuchangia mazungumzo hayo—ili tu usionekane mshamba. Hata hivyo, kwa
kweli kushiriki mazungumzo hayo kutafanya iwe vigumu zaidi kwako
kudhibiti mawazo yako. Ufanye nini? Usimame tu na kuondoka? Ndiyo, na
usione aibu kufanya hivyo! Mara nyingi inawezekana kuondoka pasipo kuonekana “mtakatifu” au kuwafanya wenzako wakucheke.
Epuka kujifurahisha kwa mambo machafu.
Bila shaka, haimaanishi kwamba sinema zote, au miziki yote ni mibaya.
Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo burudani nyingi zimekusudiwa kuamsha
tamaa zisizofaa za ngono. Biblia inatoa shauri gani? “Acheni
tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha
utakatifu katika kumwogopa Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Epuka kabisa burudani zote zinazoweza kuchochea tamaa zisizofaa za ngono.*
Tatizo la Kupiga Punyeto
Vijana fulani hujaribu kupunguza
tamaa ya ngono kwa kupiga punyeto. Lakini kufanya hivyo kunaweza
kutokeza matatizo makubwa. Biblia inawahimiza Wakristo hivi: “Viueni
viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu,
hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani.” (Wakolosai 3:5) Kupiga punyeto ni kinyume kabisa cha ‘kuua hamu ya ngono.’ Kwa kweli, kupiga punyeto huchochea na kukuza hamu hiyo!
Kupiga punyeto kwaweza kukufanya kuwa mtumwa wa tamaa zako. (Tito 3:3) Hatua moja unayoweza kuchukua ili kushinda zoea hilo ni kuzungumza na mtu unayemtumaini.
Mkristo aliyekuwa na tatizo la kupiga punyeto kwa miaka mingi anasema
hivi: “Laiti ningeweza kupata ujasiri wa kuzungumza na mtu fulani kuhusu
tatizo hilo nilipokuwa kijana! Kwa miaka mingi nilisumbuliwa na hisia
za hatia, nazo ziliathiri sana uhusiano wangu na wengine, na zaidi ya
yote, uhusiano wangu na Yehova.”
Ni nani unayeweza kuongea naye?
Mara nyingi ingefaa kuzungumza na mzazi. Au huenda Mkristo mkomavu
kutanikoni anaweza kukusaidia. Unaweza kuanza kwa kusema, “Ningependa
kuzungumza nawe kuhusu tatizo linalonisumbua sana.”
André aliongea na mzee Mkristo,
naye anafurahi kwamba alifanya hivyo. “Mzee huyo alipokuwa
akinisikiliza, alilengwa-lengwa na machozi,” André anasema.
“Nilipomaliza kuzungumza, alinihakikishia kwamba Yehova ananipenda.
Aliniambia kwamba watu wengi wana tatizo kama langu. Aliahidi kwamba
atakuwa akizungumza nami mara kwa mara kuona nimefanya maendeleo kiasi
gani na kuniletea habari zaidi kutoka katika vitabu vinavyotegemea
Biblia. Baada ya kuongea naye, niliazimia kupiga vita zoea hilo—hata
ikiwa ningeanguka mara moja moja.”
Mário aliamua kuongea na baba
yake, aliyemjali sana na kuelewa hali yake. Hata alikiri mbele za Mário
kwamba alipokuwa kijana haikuwa rahisi kwake kushinda zoea hilo.
“Nilitiwa moyo sana na mazungumzo hayo ya waziwazi na unyoofu wa baba
yangu,” asema Mário. “Nilijiambia, ikiwa alifaulu, hata mimi nitafaulu.
Niliguswa moyo sana na mtazamo wa baba yangu hivi kwamba sikujizuia
kulia.”
Kama André na Mário, wewe pia
unaweza kupata msaada wa kushinda zoea la kupiga punyeto. Hata ukijikuta
umetumbukia tena, usikate tamaa! Uwe na hakika kwamba unaweza kushinda vita hivyo.*
Dhibiti Fikira Zako
Mtume Paulo alisema: “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa.” (1 Wakorintho 9:27) Vivyo hivyo, huenda wewe pia ukahitaji kujitia nidhamu wakati
mawazo yasiyofaa kuhusu watu wa jinsia tofauti yanapoingia katika akili
yako. Mawazo hayo yakiendelea, jaribu kufanya mazoezi ya kimwili. Biblia
inasema: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo.” (1 Timotheo 4:8)
Kutembea kasi kwa muda au kufanya mazoezi ya kimwili kwa dakika chache
kwaweza kukusaidia kuondolea mbali mawazo hayo yasiyofaa.